RASIMU YA HOTUBA YA NAIBU
WAZIRI WA MAWASILIANO NA UCHUKUZI, MHESHIMIWA DR. MAUA A. DAFTARI MBUNGE YA
KUZINDUA BARAZA JIPYA LA WAFANYAKAZI LA MAMLAKA YA BANDARI TANZANIA, APRILI 12 2003, DAR
ES SALAAM
Ndugu Mwenyekiti wa Bodi
Ndugu Mwenyekiti wa Baraza
Ndugu Katibu wa Baraza
Ndugu Wajumbe wa Baraza
Ndugu Mwenyekiti,
Nashukuru sana Ndugu Mwenyekiti na Baraza lako kwa kunialika kuja kuzindua Baraza hili
jipya mlilolikamilisha kwenye uchaguzi wenu hivi karibuni.
Nimetaarifiwa katika mwaliko kwamba hii ni awamu ya nane ya Baraza la Wafanyakazi kwa
Mamlaka.
Mabaraza ya Wafanyakazi na hasa hili la Bandari, yana umuhimu wa kihistoria. Historia hiyo
kwenye taasisi nyingi imekuwa ni ya mafanikio. Baraza la bandari ni chombo chenye nafasi
pekee katika
uchumi wa kanda kubwa ya Afrika ya Mashariki na Kusini, hivyo ipo haja mnapokaa kupanga
mambo yenu, muwe na mipango thabiti mnayoweka ambayo itakuwa ni mikakati muhimu ya malengo
ya taasisi za biashara nchini na kwa majirani kwa ujumla.
Ndugu Mwenyekiti,
Umuhimu wa ushirikishwaji wa wafanyakazi unaeleweka, ingawaje ushirikishwaji wenyewe
hubadilika kila mara mazingira ya uchumi, mifumo ya uendeshaji wa taasisi, na sasa hata
utandawazi unavyoongezeka. Hivyo ushiriki wenu na menejimenti ya shirika lazima uendane na
wakati na usiwe ule wa miaka iliyopita.
Ndugu Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza,
Dunia ni biashara, na kwa dunia ya sasa ya utandawazi, mazingira yamepelekea kupanuka na
kuongezeka sana shughuli za uchumi na biashara. Utandawazi unasababisha bidhaa
zisafirishwe nchi hadi nchi kwa wingi na kwa kasi zaidi. Ili hili liwezekane, tunahitaji
kuwa
na mfumo imara wa mawasiliano na usafirishaji na pia kuondokana na urasimu katika shughuli
zenu.
Wafanyabiashara wengi, na hasa wale wa mahitaji ya kila siku wananunua toka popote pale
duniani ambapo wanaonelea kwamba bei ni nafuu kwao na huduma zao wanazipata kwa urahisi
zaidi.
Ili kukabili changamoto za maendeleo haya, bandari zitaendelea kuwa sehemu muhimu na nyeti
kwenye mtandao wa usafirishaji ulimwenguni.
Bandari hivi sasa zinatakiwa kushindana katika ubora wa huduma na wala si wingi wa shehena
tena. Ukitoa huduma bora, basi utajiuza bila jasho na shehena zitajileta zenyewe.
Ndugu Mwenyekiti,
Changamoto la mipango ya Baraza hili ni kupambana na kasi ya maendeleo ya mifumo ya
uchumi, na kuwahakikishia watumiaji wake huduma bora saa na siku zote.
Mabadiliko ya mazingira ya uchumi yanatupa changamoto ya kubadilisha mifumo ya vyombo
vyetu. Changamoto hii ndiyo iliyoleta pambazuko la ubinafsishaji. Lakini leo
hatutazungumzia chimbuko au
mantiki yake. Nyie kama wajumbe mmekwisha pata semina nyingi tu juu ya ubinafsishaji na
mnafahamu vyema suala zima, Hivyo tukubaliane tu kwamba, Mamlaka ina uzoefu na utaalamu wa
kutosha katika ubinafsishaji na mmepata nafasi ya kushirikishwa katika zoezi hili zima.
Ubinafsishaji, ndiyo dawa pekee ambayo ingeleta ubora na kiwango kikubwa cha ufanisi na
tija, bila kusahau kuongezeka kwa mtaji.
Ndugu Mwenyekiti,
Hatua za kubinafsisha shughuli za sekta ya usafirishaji wa baharini na nchi kavu sasa
zinafikia kikomo. Maandalizi yote yamekamilika na kilichosalia ni utekelezaji. Maandalizi
ya ubinafsishaji katika sekta nyingine za usafirishaji nazo zinaenda vyema kulingana na
mipango yetu; mathalani Shirika la Ndege la Tanzania tayari limekwisha binafsishwa na
ubora wa huduma zake sasa unaonekana wazi.
Pia, Kituo cha Kontena ndicho kitengo cha kwanza katika Mamlaka kubinafsishwa, na sasa
kinatumika kama kigezo cha mafanikio. Idadi ya makontena imeongezeka, masoko yanaimarishwa
na kero zilizokuwa zinatokana na urasimu wa mashirika ya umma zimeondolewa.
Kwa mujibu wa ratiba ya ubinafsishaji wa vitengo vilivyosalia kwenye Mamlaka unatarajiwa
kukamilika ifikapo Desemba, 2004 ambapo waendeshaji binafsi wanatarajiwa kupatikana.
Wakati huo Serikali itabadilisha muundo wenu. Mamlaka mpya inatarajiwa kuanza kazi Januari
2005. Mamlaka mpya inatarajiwa kupewa jukumu la kudumisha huduma za kibandari, dhamana ya
kusimamia rasilimali za bandari na kuhakikisha kuwa mikataba mbali mbali iliyowekwa ya
uendeshaji wa shughuli za bandari inafuatwa.
Ndugu Mwenyekiti,
Utaratibu na mwenendo wa ubinafsishaji wa shughuli zilizobakia umeipa Mamlaka na nyinyi
wenyewe fursa mpya iliyokosekana pale tuliposhughulikia masuala ya ubinafsishaji awamu ya
kwanza.
Naamini nafasi itakuwepo kwa Watanzania, na wafanyakazi kwa ujumla kushiriki kikamilifu
katika shughuli za uendeshaji wa vitengo
vilivyobakia. Naomba nafasi hiyo ikijitokeza muitumie kikamilifu kwa kufuata taratibu
zitakazowekwa.
Naelewa yapo maswali mawili ya msingi ambayo mgependa kujua hatima yake. Nayo ni mafao
yenu na nyumba. Napenda niwahakikishie masuala hayo yatafanyiwa kazi ipasavyo. Sina shaka
hatima njema itapatikana kwa maslahi ya wote.
Ndugu Mwenyekiti na ndugu wanabaraza,
Napenda nimalize hotuba yangu kwa kutoa nasaha chache kwenu nazo ni:
Kwanza, umuhimu wa kuhifadhi maisha yenu kwa kujikinga na balaa kubwa la gonjwa wa Ukimwi.
Janga hili limepoteza wengi wenu na litaendelea kupoteza wengine na kuacha athari mbaya
kiuchumi kwa familia na nchi kwa ujumla.
Ni muhimu sana wakati huu mkaweka mpango kabambe na kuusimamia kwa uwezo wenu wote kwa
kuendelea kujielimisha na kujikinga dhidi ya ugonjwa huu na kuhifadhi maisha yenu.
Pili, mtakumbuka Mamlaka iliwapatia nafasi ya kuwafunza namna bora ya kujiendeleza
mtakapostaafu ili muweze kuishi maisha endelevu, kwa kujizatiti na kubuni mbinu mbali
mbali za kujipatia vipato. Hivyo kumbukeni kuyatumia ipasavyo mafunzo hayo.
Tatu, ufanisi mkubwa bandarini, huleta sifa nzuri na kuwavutia washitiri kutumia bandari
zetu. Aidha ufanisi mzuri unategemea
kuwepo kwa vifaa vya kisasa na wafanyakazi wanaojituma kwa ari yao wenyewe.
Biashara ya nchi jirani, inaweza kabisa kuwa ni biashara ya nchi yetu. Kwa nchi yetu,
biashara hii ni mgodi ulioko nje ya nchi. Inafahamika kwamba mathalani Uganda inasafirisha
tani milioni moja za bidhaa zake kwenda au kutoka nchi za mbali. Katika shehena hiyo,
takwimu zenu zinaonyesha kuwa bandari zinaambulia asilimia kumi na tano tu. Kiwango kama
hicho pia kinalingana na kile kitokacho Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo.
Tujiulize hapa kwa nini karibu shehena yote toka Uganda ipitie bandari za nchi nyingine
badala ya Dar es Salaam au Tanga ama Mtwara.
Hivyo, juhudi zenu na Serikali sasa hazina budi kuelekezwa kuivutia shehena hiyo kwa
mikakati mbali mbali kama kujitangaza zaidi, kurahisishwa taratibu za uingizaji na
uondoshaji mizigo bandarini, usalama wa mizigo bandarini, kushirikiana zaidi na vyombo vya
usafirishaji, pamoja na kuimarisha mawasiliano kwa kutumia teknolojia za kisasa.
Lakini nyie kama wafanyakazi mnapaswa kuchangia zaidi kwa kuwa na mwamko wa kibiashara ya
ushindani, kinyume na ukiritimba.
Mwenyekiti,
Hatimaye basi niwatakieni heri katika majukumu yenu na hasa hili la uwakilishi katika
chombo hiki muhimu katika Mamlaka. Huenda huu ni wakati mgumu na tofauti kuliko historia
yenu ya Baraza, lakini hapana shaka safari ndefu ya mafanikio itawatulizeni kituoni salama
salimini. Baada ya kusema hayo napenda nitamke rasmi kuwa baraza lenu limezinduliwa rasmi.
HOTUBA FUPI YA MWENYEKITI WA BODI YA WAKURUGENZI
MAMLAKA YA BANDARI TANZANIA BWANA SAIDI KASSIM WAKATI WA UZINDUZI WA BARAZA KUU LA
WAFANYAKAZI APRILI 12, 2003 DAR ES SALAAM
Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi,
Dr. Maua Abeid Daftari
Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Wafanyakazi, Bwana Samson Luhigo
Ndugu Katibu, Henry Kivo
Ndugu Wajumbe,
Waandishi wa Habari na Wageni, Mabibi na Mabwana
Mheshimiwa Naibu Waziri
Kama alivyoanza Mwenyekiti wa Baraza, nami hali kadhalika napenda nikupe shukurani kwa
niaba yangu mwenyewe binafsi, na kwa niaba ya Baraza la Wakurugenzi, na ama hakika
wafanyakazi wote katika Mamlaka wanoawakilishwa na wajumbe waliopo hapa asubuhi ya leo.
Wanasiasa wanakuwa na kazi na shughuli kila siku ya maisha yao, hata wawapo likizoni, na
mwanasiasa huyo anapopewa wadhifa mwingine kama wa uwaziri, basi kama alivyosema mwenyewe
Mheshimiwa Rais, anakuwa ametwishwa uaskari, na hapa kwetu anatakiwa awe kama askari wa
mwamvuli.
Ninafurahi kwamba unaumudu uaskari wako, kwani shughuli ya leo hapa, ni mojawapo tu kati
ya mlolongo wa majukumu makubwa yanayokukabili. Kama alivyotamka Mwenyekiti wa Baraza,
juma hili linawamalizia ngwe mliyokuwa nayo huko Bungeni Dodoma.
Mimi binafsi, nimefurahi kwamba umeweza kuwepo hapa, kwani, kazi yote inayofanyika katika
Baraza hili, hatima yake ni mapendekezo yanayoletwa kwenye Bodi ya Wakurugenzi. Na Bodi
nayo, itakapomaliza kazi ya kuzichambua hoja zitakazotoka hapa, inapendekeza kwa Wizara
yetu ya Mawasiliano na Uchukuzi ambayo unaiongoza wewe.
Tunafarijika sana kwamba kwa vipindi vyote, vyombo vyote vya Mamlaka, yaani Baraza hili,
na Bodi yangu, vimeweza kupendekeza mipango ambayo yalipofika mbele yako, imepokelewa na
kuidhinishwa.
Sisi katika Bodi tunalitazama Baraza hili kama chombo cha ufanisi, kwani limetuwezesha
kufanya kazi na dhamana tuliyokabidhiwa ya chombo hiki kwa ufanisi na imani
ilivyotarajiwa. Ningependa kuchukua fursa hii kumpongeza mwenyekiti wao na wajumbe kwa
ujumla na papo hapo kuwasihi wasije wakabweteka, na kulegeza kamba, hata hapo muundo wa
Mamlaka utakapokuwa umebadilika kabisa.
Ama kwa hakika nitoe tahadhari hapa kwamba pamoja na kwamba wamesema wamekuwa wakifanya
kazi zao kuiushindani ndani ya mfumo wa ukiritimba, ushindani katika soko huria ni mkubwa
na mgumu zaidi.
Baraza halina budi kujipima na kuhakikisha kwmba linaziba mapendgo yoyote yale miongoni
mwao yatakayobainika kuwa ni udhaifu hapo wanapoingia kwenye vita vya biashara huria.
Mheshimiwa Naibu Waziri
Kazi yangu hapa ni kukukaribisha kwenye hadhara, hivyo nisiseme mengi bali tu nikuahidi
kwamba tayari tupo kwenye kipindi cha kuandaa mipango ya mamlaka kwa kipindi kijacho, na
juma lijalo tutakuwa tumeikamilisha na kuiwasilisha kwenu kwa wakati unaotakiwa kisheria.
Mheshimiwa
Karibu hadhara hii ya wajumbe ni yako wewe sasa.
HOTUBA YA MWENYEKITI WA BARAZA KUU LA WAFANYAKAZI WA MAMLAKA YA BANDARI
BWANA SAMSON M.E. LUHIGO WAKATI WA UZINDUZI WA BARAZA APRILI 12, 2003
DAR ES SALAAM
Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi,
Dr. Maua Abeid Daftari
Mwenyekiti wa Bodi Bwana Saidi Kassim
Ndugu Katibu, Henry Kivo
Ndugu Wajumbe,
Waandishi wa Habari na Wageni, Mabibi na Mabwana
Mheshimiwa Naibu Waziri,
Kwa niaba ya Baraza hili, ninapenda kuelezea furaha na shukrani zetu kwako wewe binafsi,
Serikali na hasa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi kutupa fursa na heshima na muda wako
kuzungumza na moja ya vyombo muhimu sana kwenye Mamalaka ya Bandari Tanzania, yaani Baraza
la Wafanyakazi.
Tunafahamu kuwa majukumu mliyonayo kwenye ofisi zenu wenyewe ni mazito na makubwa lakini
pamoja na yote hayo, imepatikana nafasi ya kuja hapa na kutupa mwangaza wa kutazama wajibu
tulio nao kama Mamlaka.
Nikisema uzito wa kazi zenu, ninazingatia kwamba kwa majuma mawili sasa Bunge limekuwa
likikutana na Wizara yako hasa, na imekuwa na muswada mzito wa uanzishaji wa Mamlaka ya
Uthibiti wa Mawasiliano (Communications Regulatory Authority).
Mheshimiwa Naibu Waziri,
Kisha kutoa shukurani kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya wajumbe wa Baraza, napenda
kuelekeza mtazamo wangu kwenye dhima ya Baraza la Wafanyakazi, na Mamlaka ya Bandari.
Hii ni awamu ya nane ya miaka mitatu mitatu ya Baraza hili. Mamlaka imekuwa mbele katika
utekelezaji wa agizo la Serikali la miaka thelathini na zaidi ya ushirikishwaji wa
wafanyakazi kwenye kuweka wenyewe mipango ya uchumi ya shirika walilodhaminiwa
kuliendesha, tangu lilipoanzishwa, mwaka 1977.
Hili ni Baraza Kuu. Linakuwa Kuu kutokana na kuwepo katika Mamlaka vituo vikuu vitatu vya
kazi ambavyo ni Makao Makuu, na Bandari tatu za Dar Es Salaam, Tanga na Mtwara. Muundo
katika kila baraza la kituo ni wa vikundi vitatu vya wafanyakazi. Kwanza ni Menejimenti
ambao huingi a katika baraza kwa mujibu wa ofisi zao, na pili ni chama cha wafanyakazi
ambao huwakilishwa na viongozi wake akiwemo mwenyekiti na katibu wake. Kundi la tatu ni
wawakilishi wa wafanyakazi ambao huchaguliwa na wafanyaakazi kutokana na idara zao.
Baraza Kuu linaundwa na Menejimenti kutoka kituo cha Makao Makuu, Vuingozi wa vituo vyetu
vitatu, viongozi wa vyama vya wafanyakazi katika vituo vyote, na wawikilishi wa
wafnayakazi waliochaguliwa toka kwenye mabara ya vituo.
Vyombo vya kazi katika mabaraza yote ni Kamati za utendaji na Baraza Kuu lenyewe. Kamati
ya Utendaji inafanya kazi kubwa ya kupitia mapendekezo ya vituo kisha kuyawasilisha kwenye
baraza kuu.
Mwaka huu, tumekuwa na upungufu kidogo katika kuanza kwa shughuli za Baraza . Kutokana na
mtazamo mpya wa wafanyakazi, wameamua kuunda chama kipya kinachojumuisha wafanyakazi wa
bandarini pekee, yaani dockworkers, na kujitoa katika fungamano la awali la vyombo vya
mawasiliano.
Taratibu zao za kujiandikisha zimewachukua muda na hadi. Uwakilishi wao katika kipindi
hiki, kwa vituo ambavyo tayari vilikuwa vimejitoa kisheria na chama chao, haukuwezekana
isipokuwa kwa bandari ya Dar Es Salaam.
Hata hivyo tunatarajia kwamba tutawapata washiriki hao katika vikao vijavyo vya baraza.
Kazi ya Baraza katika vikao vyake vinavyofanyika mara mbili kila mwaka wa fedha ni
kujadili malengo, faida na matumizi ya kutokana na matarajio ya shehena na pato letu.
Mamlaka ina malengo thabiti manne makuu ya kazi zetu, ambayo ni; mosi kuendelea na
utekelezaji wa zoezi la ubinafsishaji, pili kutoa huduma kwa ufanisi kwa wateja wetu kila
wakati, tatu kupata ziada ya kutosha kulingana na rasilimali iliyopo, na nne kulinda idadi
sahini ya wafanyakazi wenye ujuzi kikamilifu na ari.
Katika malengo haya yapo matatizo mengi, lakini mimi ningependa kuyaita ni
challenges. Baraza hili linayapitia matatizo haya na mikakati iliyotayarishwa
ya kuyakimu, na ningependa nitaje tu hapa kwamba nyakati zote limeweza kuishauri
menejimenti na bodi kwa ufanisi mkubwa.
Baraza limekuwa likiendesha shughuli zake kwa mihula yote hiyo kwenye mfumo wa ukiritimba
na kama taasisi ya Umma. Pamoja na ukiritimba, naweza kukiri kwamba wakati wote tumekuwa
na mtazamo halisi wa ushindani na kuwa na mafanikio makubwa.
Lakini mtazamo wa biashara na uchumi hivi sasa umebadilika na baraza halina budi kufuata
dira hiyo hiyo.
Mfumo wa Mamlaka hivi sasa unafanyiwa marekebisho sambamba na uhuishwaji wa shughuli za
uchumi na sekta binafsi. Kwa mwendo huo hapana shaka huu ni muongo wa mwisho wa mfumo huu
wa Baraza kwa Mamlaka ya Bandari. Mabaraza yafuatayo, japo yatakuwa bado ni ya uchumi,
yatakuwa na malengo tofauti na sasa.
Tayari sehemu muhimu zaidi kiuchumi na utendaji kazi Kitengo cha Makontena
kimekwisha pangishwa yapata miaka mitatu na zaidi.
Hali ya utendaji katika kitengo hicho kama tunavyoifuatilia ni ya kuridhisha, na
mwendeshaji huyo Tanzania International Container Terminal Services Ltd., (TICTS)
ameweza kuendeleza na kuboresha misingi mizuri ya kazi na vitendea kazi alivyorithi toka
Mamlaka.
Kazi ya ubinafsishaji iliyobakia ni ile ihusuyo kitengo cha shehena za kawaida na zile
huduma nyingine za kibiashara kwenye bandari ya Dar es Salaam pamoja na bandari za Tanga
na Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Waziri,
Katika hatua zitakazofuata za ubinafsishaji vitengo vilivyosalia, Mamlaka imelenga vyema
na inawaandaa wafanyakazi kupata fursa ya kushiriki kama wawekezaji.
Mheshimiwa Naibu Waziri,
Naomba nishukuru tena na nimuombe Mwenyekiti wetu wa Bodi, Mzee Saidi Kassim achukue fursa
yake rasmi kukukaribisha uweze kuzungumza na wajumbe.
Top